UHALIFU NCHINI ZA SADAC UPIGWE VITA
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo
ya Ndani ya Nchi, Balozi Hassan Simba Yahya, amewaomba washiriki wa
Mkutano wa Kamati Ndogo ya Usalama wa raia wa Jumuiya ya Maendeleo
Kusini mwa Afrika (SADC), kuhakikisha wanapambana kupunguza vitendo vya
ujangili, biashara ya magendo, biashara ya binadamu, na uhamiaji haramu
kwani vitendo hivyo vinarudisha nyuma maendeleo ya nchi zilizopo katika
jumuiya hiyo, na kusababisha kuzorota kwa shughuli za maendeleo na
uchumi.
NUKUU "Hatuwezi kuendelea kiuchumi katika nchi zetu wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, kama matendo ya ujangili,biashara ya binadamu, masuala ya wakimbizi, uhamiaji haramu hayajatafutiwa ufumbuzi, kwani haya yatazorotesha shughuli za kiuchumi ikiwepo utalii, hivyo ni bora tukayafanyia kazi maeneo hayo," alisema Balozi Simba.
Akizungumza wakati wa uchangiaji mada katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Jorge Cardoso, alisema uhalifu katika mipaka ya nchi wanachama ikiwemo uwindaji haramu wa pembe za ndovu, uhamiaji haramu,biashara ya binadamu na madawa ya kulevya lazima vidhibitiwe kwani vikiachwa mbeleni vitahatarisha Amani na utulivu uliopo katika nchi wanachama.
"Amani na utulivu katika nchi wanachama ni kichocheo cha mabadiliko ili kupiga hatua za kimaendeleo kwenda mbele na kushirikiana kukuza uchumi katika nchi wanachama wa SADC, hivyo yatupasa wote kwa pamoja kuunga mkono harakati za kukomesha vitendo vya uhalifu katika nchi na mipaka yetu," alisema Cardoso.
Aidha washiriki wa mkutano huo kutoka katika nchi za Tanzania, Afrika Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Swaziland, Malawi, Zimbabwe kwa pamoja walikubaliana kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama katika nchi zao kudhibiti matendo yote yanayohatarisha amani na utulivu.
No comments: